SERMONS

MWANZO WA AGIZO LA KUSHIKA SABATO NA SABABU ZAKE

  Kabla ya kujifunza kwa undani sana, juu ya mwanzo wa agizo la kushika sabato na sababu zake, kwanza ni vema tukajifunza nini maana halisi ya neno Sabato. Neno ‘Sabato’ ambalo kwa kiingereza ni ‘Sabbath’ linatokana na neno la Kiebrania ‘Shabbath’ likiwa na maana ya ‘Pumziko’ au ‘kustarehe na kuacha kazi.’ Kwa Kiyunani huitwa ‘Sabbaton.’ Na neno hili halimaanishi siku ya kuabudu, bali ni pumziko la kazi.
  Asili ya sabato yaani pumziko la kazi, inapatikana katika kitabu cha Mwanzo, pale Mungu alipomaliza kazi yake ya uumbaji na kupumzika siku ya saba (Mwanzo 2:1-3). Pamoja na Mungu kupumzika siku ya saba, lakini bado Biblia haituambii kama Mungu aliwaagiza Adam na Hawa kupumzika siku ya saba. Kadhalika maandiko hayatuoneshi kama Nuhu, Ibrahimu, Isaka na Yakobo walifundishwa juu ya sheria ya kupumzika siku ya saba (sabato).
  Agizo la kwanza kwa wanadamu, la kushika sheria ya kushika siku ya sabato, lilitolewa na Mungu mwenyewe kwa Wana wa Israeli tu, na kwa mkono wa Musa. Ni dhahiri kabisa, hata Israeli mwenyewe yaani Yakobo, wakati akiwa hai, hakuwahi kusikia habari ya kupumzika siku ya saba (sabato). Agizo hili halikutolewa kwa mataifa mengine, bali kwa wana wa Israeli tu, na sababu kuu ni kwamba, kwa kipindi hicho, ni wana wa Israeli peke yao ndiyo waliokuwa wanamjua Mungu wa kweli yaani Yehova. Ni kwa sababu hiyo basi, Mungu aliwapa sheria (Torati) watu wake, yaani Amri kumi, sheria nyingine 613 na Hukumu zake. Katika kitabu cha Kumbukumbu la Torati 4:7-8 Biblia inasema, “Kwa maana liko taifa gani kubwa, lililo na Mungu aliye karibu nao, kama Bwana, Mungu wetu, alivyo, kila tumwitapo? Tena liko taifa gani kubwa, lililo na amri na hukumu zenye haki kama torati hii yote, ninayoiweka mbele yenu leo.”  Lakini pia Musa mwenyewe alithibisha kwamba, sheria ya kushika siku ya sabato na sheria nyingine haikuanza na baba zao, bali ilianza na wao wenyewe yaani wana wa Israeli; katika Kumbukumbu la torati 5:1-3 Biblia inasema, “Musa akawaita Israeli wote, akawaambia, Enyi Israeli, zisikieni amri na hukumu ninenazo masikioni mwenu leo, mpate kujifunza na kuangalia kuzitenda. Bwana Mungu wetu, alifanya agano nasi katika Horebu. Bwana hakufanya agano hili na baba zetu, bali na sisi, yaani sisi sote tulio hapa, tu hai.”   Wapo baadhi ya washika sheria ya siku ya sabato wa nyakati za leo, ambao hutoa madai ya kwamba, Adamu alikuwa ni msabato wa kwanza. Kigezo wanachotumia, ni kwa sababu Mungu alipumzika siku ya saba, hivyo husema kwamba, Adamu naye alipumzika ingawa Biblia haituambii kama Adamu alipumzika. Na kama alipumzika, alipumzika kwa sababu ya kazi ipi aliyoifanya? Maana kazi ya uumbaji ilifanywa na Mungu peke yake. Musa ambaye ndiye aliyekuwa msabato halisi, anaipinga hoja hii katika mistari tuliyosoma hapo juu kwa kusema kwamba, Mungu hakufanya agano la zile sheria na baba zao, bali wao wenyewe. Kwa hiyo ni wazi kabisa, kuanzia Adamu mpaka Yakobo hawakuwahi kuambiwa na Mungu juu ya sheria ya kushika siku ya sabato.

SABABU ZILIZOPELEKEA WANA WA ISRAEL KUPEWA
SHERIA YA KUSHIKA SABATO
   Ziko sababu kuu mbili zilizopelekea wana wa Israeli peke yao, kuamriwa kushika sabato;
1.   NI KUMBUKUMBU KWA WANA WA ISRAELI KUWA WALIKUWA WATUMWA KATIKA NCHI YA MISRI.
Katika kitabu cha Kumbukumbu la torati 5:15 Biblia inasema, “Nawe utakumbuka ya kuwa wewe ulikuwa mtumwa katika nchi ya Misri, na ya kuwa Bwana, Mungu wako, alikutoa huko kwa mkono wenye nguvu, na mkono ulionyoshwa, kwa sababu hiyo Bwana, Mungu wako, alikuamuru ushike sabato.’’ Kwa hiyo, ni wana wa Israeli peke yao, ndiyo walio amriwa kushika sheria ya siku maalum ya kupumzika yaani sabato, ili kwao iwe kumbukumbu kwamba, walikuwa watumwa katika nchi ya Misri. Kwa hiyo, kwa mtu asiye Mwana wa Israeli akishika sheria ya siku ya sabato, atakuwa anakumbuka nini? Je alishawahi kuwa mtumwa huko Misri?

2.   WANA WA ISRAELI WALIAMRIWA KUISHIKA SABATO ILI IPATE KUWA ISHARA YA AGANO KATI YAO NA MUNGU.
Katika kitabu cha Kutoka 31:13 Biblia inasema, “Kisha, nena wewe na wana wa Israeli, na kuwaambia, Hakika mtazishika sabato zangu, kwa kuwa ni ISHARA kati ya mimi na ninyi, katika vizazi vyenu vyote, ili mpate kujua ya kuwa mimi ndimi Bwana niwatakasAye ninyi.” Kadhalika katika kitabu cha Kutoka 31:16-17 Biblia inasema, “Kwa ajili ya hayo wana wa Israeli wataishika sabato, kuiangalia sana hiyo, katika vizazi vyao vyote, ni agano la milele. Ni ISHARA kati ya mimi na wana wa Israeli milele…..” Pia katika Ezekieli 20:20 Neno la Mungu linasema, “Zitakaseni sabato zangu, nazo zitakuwa ISHARA kati ya mimi na ninyi, mpate kujua ya kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.” Ezekiel 20:12 inasema, “Tena naliwapa sabato zangu, ziwe ISHARA kati yangu mimi na wao…..

ANGALIZO: Neno ishara linamaanisha siyo kitu halisi, bali ni kitu kinacho ashiria kitu fulani ambacho kitakuja, ni kitu kinachoelekeza kitu fulani halisi ambacho kitakachokuja. Sabato ilikuwa ikiashiria pumziko halisi ambalo Bwana Yesu amekuja kuwapa watu duniani, na ndiyo sababu ya Yeye kujiita Bwana wa pumziko (sabato) (Luka 6:5) akimaanisha kuwa Yeye ndiye mtoa pumziko.  Roho Mtakatifu kupitia Mtume Paulo, amefafanua katika kitabu cha Wakolosai kuwa, sabato ilikuwa ni kivuli cha mambo yajayo. Sabato ilikuwa siyo kitu halisi na ndiyo maana mtu akisha pata kitu halisi hawezi tena kung’ang’ania ishara au kivuli (negative). Wakolosai 2:16-17 inasema, “Basi, mtu asiwahaukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au SABATO; mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo.
  
IDADI YA SABATO AMBAZO WANA WA ISRAELI WALIAMRIWA
KUZISHIKA NA MALENGO YAKE
   Katika kushika sheria ya sabato, Wana wa Israeli hawakupewa sabato moja tu, yaani sabato ya siku, kama wanavyofanya wanaojiita wasabato wa leo. Kwa mtu mwenye ufahamu sahihi wa maandiko, anaweza akahoji maswali mengi, na ya msingi sana dhidi ya wanaoshika sabato katika nyakati za leo. Kabla hatujaingia kwa undani zaidi, ebu tuangalie idadi ya sabato ambazo wana wa Israeli waliamriwa kuzishika. Katika kitabu cha Walawi 26:2 Neno la Mungu linasema, “Zishikeni SABATO ZANGU, na kupastahi patakatifu pangu; mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.” Tunaona hapa Mungu anatumia neno ‘sabato zangu’ na siyo ‘sabato yangu’. Tukiangalia katika Ezekieli 20:20 Biblia inasema, “Zitakaseni SABATO ZANGU; nazo zitakuwa ishara kati ya mimi na ninyi, mpate kujua ya kuwa mimi ndimi Bwana, Mungu wenu.” Tunaona na hapa Mungu anatumia ‘sabato zangu’ na siyo ‘sabato yangu’. Katika kitabu cha Kutoka 31:13 inasema, “Kisha, nena wewe na wana wa Israeli, na kuwaambia, Hakika mtazishika SABATO ZANGU, kwa kuwa ni ISHARA kati ya mimi na ninyi, katika vizazi vyenu vyote, ili mpate kujua ya kuwa mimi ndimi Bwana niwatakasaye ninyi.” Kadhalika na hapa Mungu anatumia neno ‘sabato zangu’ na siyo ‘sabato yangu’. Pia katika kitabu cha Walawi 19:30 Biblia inasema, “Zishikeni SABATO ZANGU, mpaheshimu patakatifu pangu; mimi ndimi Bwana.” Na hapa pia tunaona Mungu anatumia neno ‘sabato zangu’ na siyo ‘sabato yangu’. Kwa hiyo, hii inatuthibitishia wazi kabisa kwamba, Mungu hakuawaagiza wana wa Israeli kushika sabato moja ya siku kama wanavyofanya wanaojiita wasabato wa leo.

IDADI YA SABATO ZILIZOAMRIWA NA MUNGU ILI
WANA WA ISRAELI WAZISHIKE
Kulingana na maandiko, wana wa Israeli walipewa sabato zaidi ya moja, zifuatazo ni baadhi ya sabato hizo;
1.   SABATO YA SIKU.
Sabato ya siku ni pumziko ambalo lilifanywa baada ya siku sita za kazi, hivyo siku ya saba, walipewa amri ya kupumzika, kama tunavyoweza kuiona katika amri ya nne miongoni mwa amri kumi. Katika kitabu cha Kutoka 35:2 Biblia inasema, Fanyeni kazi siku sita, lakini siku ya saba itakuwa siku takatifu kwenu; ni sabato ya kustarehe kabisa kwa Bwana, mtu awaye yote atakayefanya kazi yoyote katika siku atauawa.”  (Soma pia Kutoka 31:14-15; Kumbukumbu 5:14).

2.   SABATO YA MWAKA.
Sabato ya mwaka ni pumziko ambalo lilifanywa baada ya miaka sita ya kazi, hivyo mwaka wa saba, wana wa Israeli walipewa amri ya kupumzika mwaka mzima. Tunaweza kuona sabato hii katika kitabu cha Walawi 25:1-5, “Kisha Bwana akanena na Musa katika mlima wa Sinai, na kumwambia. Nena na wana wa Israeli, hapo mtakapoingia katika nchi niwapayo, ndipo hiyo nchi itashika sabato kwa ajili ya Bwana. Panda shamba lako miaka sita, na miaka sita lipalie shamba lako la mizabibu, na kuyachuma matunda yake; lakini katika mwaka wa saba itakuwa ni sabato ya kustarehe kwa ajili ya hiyo nchi, ni sabato kwa Bwana; usipande shamba lako wala usipalie shamba lako la mizabibu. Hicho kimeacho chenyewe katika mavuno yako, usikivune, wala zabibu za mizabibu isiyopelewa usizitunde, UTAKUWA MWAKA WA KUSTAREHE KABISA KWA AJILI YA NCHI HIYO. Na hiyo sabato ya nchi itakuwa chakula kwenu; kwako wewe,  na kwa mtumwa wako, na kwa mjakazi wako, na kwa mtumishi aliyeajiriwa, na kwa mgeni wako akaaye pamoja nawe.”

3.   SABATO YA SABATO SABA ZA MIAKA (YUBILEE)
Sabato hii ni pumziko ambalo lilifanywa baada ya sabato saba za miaka yaani miaka saba mara saba unapata miaka 49, hivyo mwaka wa hamsini, wana wa Israeli waliamriwa kupumzika. Kwa jina lingine iliitwa Yubile. Sabato hii tunaweza kuiona katika kitabu cha Walawi 25:8-11, “Nawe utajihesabia sabato saba za miaka, maana, miaka saba mara saba; zitakuwa ni siku za sabato saba za miaka kwenu, maana miaka arobaini na kenda (49).Ndipo utakapoipeleka pande zote hiyo baragumu, yenye sauti kuu, siku ya kumi ya mwezi wa saba; katika siku hiyo ya upatanisho mtaipeleka baragumu katika nchi yenu yote. NA MWAKA WA HAMSINI MTAUTAKASA, na kupigwa mbiu ya kuachwa mahuru katika nchi yote kwa watu wote waiketio, itakuwa ni yubile kwenu; nanyi kila mtu atairudia milki yake mwenyewe, nanyi mtarejea kila mtu kwa jamaa yake. Mwaka huo wa hamsini utakuwa ni yubile kwenu; MSIPANDE MBEGU, WALA MSIVUNE, KITU HICHO KIMEACHO CHENYEWE, WALA MSIZITUNDE ZABIBU YA MIZABIBU ISIYOPELEWA.”
  Ebu mtoto wa Mungu sasa tujiulize swali, kama kweli wasabato wa leo wako sahihi kushika sabato, kwa nini wanashika sabato ya siku peke yake? Je mbona hizi nyingine zimewashinda? Kama sabato inayoshikwa leo na wasabato, msingi wake ni Biblia, mbona hizi sabato nyingine wameziacha na wakati zote ziliamriwa na Mungu mwenyewe? Hata hivyo Neno la Mungu katika kitabu cha Yakobo 2:10 inasema, “Maana mtu awaye yote atakaye ishika sheria yote, ila akajikwaa katika neno moja, amekosa juu ya yote.” Kwa hiyo kama wasabato wa leo wanashika sabato ya siku tu, na kuacha sabato nyinginezo, ni wazi kabisa wamekosa juu ya yote.

MALENGO YA KUSHIKA SABATO KWA WANA WA ISRAELI
  Lengo la kushika sabato kwa wana wa Israeli lilikuwa ni kupumzika kazi na kustarehe tu na wala si vinginevyo. Wanaojiita wasabato katika nyakati za leo, wameigeuza sheria hii ya kushika sabato kama ni siku ambayo Mungu ameamuru wafanye ibada, kinyume kabisa na kusudi zima na maana halisi ya neno sabato. Watu hawa wamekuwa wakishutumu wakristo wengine na kusema kuwa, Jumamosi ndiyo siku halali ya kufanya ibada, lakini Jumapili, ni siku ambayo haikuamriwa na Mungu, watu kukusanyika kufanya ibada. Ni vema ifahamike kuwa agizo la kushika sabato na siku ya kukusanyika ni vitu viwili tofauti na ni maagizo mawili tofauti ambayo wana wa Israeli walipewa kuyatekeleza. Katika agizo la kukusanyika kwa wana wa Israeli, Mungu alitoa siku mbili yaani Jumapili na Jumamosi, ingawa wasabato karibu wote hawalijui jambo hili, maana hao wamekaririshwa siku ya sabato tu yaani Jumamosi. Tunaweza kuthibitisha ukweli huu katika kitabu cha Kutoka 12:16 Biblia inasema, “SIKU YA KWANZA kutakuwa kwenu na kusanyiko takatifu, na SIKU YA SABA kutakuwa na kusanyiko takatifu, haitafanywa kazi yoyote katika SIKU HIZO, isipokuwa kwa hiyo ambayo kila mtu hana budi kula, hiyo tu ifanyike kwenu.” Mungu aliwaamuru wana wa Israeli wakusanyike siku ya kwanza ya juma yaani Jumapili na siku ya saba yaani Jumamosi kwa kalenda ya kwetu. Pia Mungu hakuwaagiza kukusanyika tu, bali aliwaagiza wasifanye kazi pia. Lakini wanaojiita wasabato nyakati za leo, wanapinga kukusanyika Jumapili sawasawa na maagizo ya torati wanayodai kuifuata. Swali ni kwamba, mafundisho yao ya kukusanyika siku ya sabato yametoka wapi? Kama ni kwenye Biblia mbona siku moja hii wameiacha? Je aliyetoa agizo la siku ya sabato ni Mungu mwingine na aliyetoa agizo katika kitabu cha Kutoka 12:16 (yaani kukusanyka siku ya Jumapili) ni Mungu mwingine?
   Kwa hiyo agizo la kukusanyika lilikuwa ni siku mbili, imetajwa ya kwanza ni Jumapili (siku ya kwanza ya juma) na ya pili ni Jumamosi (siku ya saba) kwa kalenda yetu, kama tulivyoona katika kitabu cha Kutoka 12:16. Sasa tukija kwenye agizo la kushika sabato halikuwa ni siku ya kukusanayika, bali ni pumziko la kazi tu na kustarehe kama tunavyoweza kuona katika kitabu cha Kutoka 31:14-15, “Basi mtaishika hiyo sabato; kwa kuwa ni takatifu kwenu; kila mtu atakayeitia unajisi hakika yake atauawa; kwa kuwa kila mtu afanyaye kazi siku hiyo, nafsi hiyo itakatiliwa mbali na watu wake. Kazi itafanywa siku sita; lakini siku ya saba ni sabato ya kustarehe kabisa, takatifu kwa Bwana, kila mtu atakayefanya kazi yoyote katika siku ya sabato, hakika yake atauawa.” Mungu hapa anasema kila mtu atakayefanya kazi siku hiyo atauawa, hajasema kila mtu atakaye kosa kwenda kwenye kusanyiko atauawa. Na ndiyo maana kwenye Biblia, inapotaja neno sabato ina maana ya kupumzika kazi na siyo kufanya kusanyiko la kuabudu kama wafanyavyo wanaojiita wasabato wa leo. Pia Kutoka 35:2 Biblia inasema, “Fanyeni kazi siku sita, lakini siku ya saba itakuwa siku takatifu kwenu; ni sabato ya kustarehe kabisa kwa Bwana; mtu awaye yote atakayefanya kazi yoyote katika siku hiyo atauawa.” Tunaona tena hapa, Mungu anasisitiza kwamba, atakayeuawa, ni yule atakayefanya kazi siku ya sabato, na hakusema atakayekosa kwenda kukusanyika kwa ajili ya ibada, kwani agizo hili lilihusiana na kupumzika kufanya tu. Kimsingi unaposema sabato, siyo dhehebu, wala siyo siku ya kuabudu, bali ni pumziko la kazi. Nyakati za leo, wanaojiita wasabato, wanachanganya siku ya kusanyiko na siku ya pumziko la kazi. Tukiangalia tena maandiko katika kitabu cha Kumbukumbu la torati 5:14 kwenye ile amri ya nne ya kushika sabato, Biblia inasema, “Lakini siku ya saba ni sabato ya Bwana, Mungu wako; siku hiyo usifanye kazi yoyote, wewe, wala mwanao, wala binti yako, wala mtumwa wako, wala mjakazi wako, wala ng’ombe wako, wala punda wako, wala mnyama wako yeyote, wala mgeni aliye ndani ya malango yako, ili mtumwa wako na mjakazi wako wapumzike vile vile kama wewe.” Kadhalika na hapa Mungu anaifafanua kwa uzuri kabisa, maana ya sabato na lengo lake. Lengo lilikuwa watu wapumzike, wanyama wapumzike, wafanyakazi wapumzike na kustarehe, kwa sababu hiyo, sabato iliwagusa mpaka wanyama. Kama ingekuwa kwamba sabato ilimaanisha siku ya kuabudu basi wanyama wasingetajwa kupumzika.
   Mtu aliyepigwa mawe hata kufa nyakati za Musa jangwani, hakuuawa kwa sababu hakwenda kuabudu siku ya sabato, bali aliuawa kwa sababu alifanya kazi (Hesabu 15:32-36). Hii inathibitisha kwamba agizo la kushika sabato lililenga pumziko la kazi tu na si agizo la kukusanyika kama wanavyodai wasabato wa leo. Wana wa Israeli walikusanyika siku ya saba (Jumamosi) na siku ya kwanza ya juma (Jumapili) kwa agizo la Mungu mwenyewe katika Kutoka 12:16, kama tulivyokwisha kuona hapo nyuma. Kimsingi ni kwamba, katika amri kumi (Kumbukumbu 5:12-15), amri ya nne inazungumzia kupumzika kazi tu. Na Kutoka 12:16 Mungu anatoa mwongozo wa siku za kukusanyika kwa ibada. Swali ni kwamba, wasabato wa leo wanakusanyika Jumamosi kwa msingi wa andiko lipi kati ya hayo? Kama kwa msingi wa amri ya nne ya kushika sabato (Kumbukumbu 5:12-15), basi watakuwa wamepotea, maana pale haikuzungumziwa siku ya kukusanyika kwa ajili ya ibada, bali ni pumziko la kazi tu. Lakini kama wana kusanyika Jumamosi, kwa msingi wa andiko la Kutoka 12:16, kadhalika watakuwa wamepotea, maana, katika siku za kukusanyika, katika andiko hili, Mungu ametoa siku mbili yaani siku ya kwanza ya juma (Jumapili) na siku ya saba ya juma (Jumamosi), sasa mbona siku ya kwanza ya Juma (Jumapili) wanaipinga? Ni wazi kabisa wanampinga Mungu.

ANGALIZO: Ili kupata pumziko vizuri siku ya sabato, wana wa Israeli waliagizwa na Mungu, wasitoke mahali pao; Kutoka 16:29 Biblia inasema, “Angalieni, kwa kuwa BWANA amewapa ninyi hiyo sabato, kwa sababu hii huwapa siku ya sita chakula cha siku mbili; kaeni kila mtu mahali pake, mtu awaye yote asiondoke mahali pake kwa siku ya saba. Basi hao watu wakapumzika siku ya saba.” Kwa hiyo, nyakati zile, ilikuwa ni sheria kwa wana wa Israeli, kutotembea mwendo mrefu siku ya sabato. Walitembea mahali pafupi sana, na hatimaye urefu ule wakauita mwendo wa sabato (Matendo 1:12). Wanaojiita wasabato wa leo, siku ya Jumamosi, wanatembea mwendo zaidi ya kilometa moja, kwenda kanisani, je hii ni kweli sabato ya kweli (pumziko la kweli)?

HOJA ZA WASABATO DHIDI YA WAKRISTO WENGINE
NA MAJIBU YAKE
   Zipo hoja nyingi ambazo hutolewa na wanaojiita wasabato katika nyakati za leo, kuhusiana na siku ya Jumapili, lakini zifuatazo ni baadhi tu ya hoja hizo na majibu yake;
1. Wasabato hudai kwamba, Wakristo wanaofanya ibada zao siku ya jumapili, ni makosa mbele za Mungu, maana siyo agizo la Mungu bali ni agizo la mwanadamu.
  
   Hoja hii si ya msingi na haina ukweli ndani yake. Kwanza kabisa ningependa watu waelewe kwamba, Wakristo wanaofanya ibada zao siku ya jumapili na siku nyingine, hao si wanafunzi wa Musa, bali ni wanafunzi wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye ndiye mdhamini wa agano lililo bora zaidi, yaani agano jipya, kama Biblia inavyosema katika Waebrania 7:22, “Basi kwa kadiri hii Yesu amekuwa mdhamini wa agano lililo bora zaidi.” Lakini pia, msingi wao, wa kufanya ibada siku ya Jumapili na siku nyingine, hautokani na torati ya Musa, bali ni msingi unaotoka kwa Bwana wetu Yesu Kristo (nitaeleza kwa upana katika sura inayosema ‘Kwa nini Wakristo wanafanya ibada zao siku ya Jumapili’). Hata hivyo, bado katika agano la kale Mungu aliagiza watu wakusanyike Jumapili ingawa wasabato wengi hawalioni andiko hilo. Tukiangalia katika Kutoka 12:16 Biblia inasema, “SIKU YA KWANZA kutakuwa kwenu na kusanyiko takatifu, na SIKU YA SABA kutakuwa na kusanyiko takatifu, haitafanywa kazi yoyote katika SIKU HIZO, isipokuwa kwa hiyo ambayo kila mtu hana budi kula, hiyo tu ifanyike kwenu.” Siku ya kwanza ya juma ni Jumapili, na siku ya saba ni Jumamosi kwa kalenda yetu. Kwa hiyo mtoto wa Mungu, mwanafunzi yeyote wa Musa wa nyakati za leo anapokuja na kukusumbua juu ya siku ya Jumamosi, mwambie mbona siku ya kwanza ya juma yeye hafanyi ibada na ni agizo la Mungu kama tulivyokwisha kuona katika Kutoka 12:16.
2. Wasabato wa leo wanadai kwamba, Wakristo wanafanya kusanyiko siku ya Jumapili, wana abudu mungu Jua, kwa sababu siku ya Jumapili kwa Kiingereza huitwa ‘Sunday’ ikimaanisha siku ya Jua.

   Hoja hii si ya msingi na haina ukweli ndani yake. Ili tupate kuelewa ukweli wenyewe, kwanza ni vema tukaziorodhesha siku zote saba kwa kiingereza alafu tuangalie maana ya siku zote saba, hapo ndipo tutabaini ukweli. Lakini ni vema tukafahamu kuwa, siku hizi saba, zilipewa majina na wapagani wa Kirumi kulingana na mungu wa kila siku hiyo, ingawa Mungu alipoumba siku, hakuzipa majina, bali alitumia siku ya kwanza hadi siku ya saba. Hivyo kuzipa kwao majina ya miungu yao ya kipagani, haizuii Wakristo wa kweli kumuabudu Mungu wao aliyeumba siku hizo, maana Yeye ndiye Mzee wa siku. Kwa mfano, siku inapoitwa, siku ya Nyerere (Nyerere day) ikiangukia Jumamosi, je tutasema wasabato wanamwabudu Mwalimu nyerere, na hivyo kuwafanya wasifanye ibada siku hiyo? Kwa sababu serikali imetangaza siku hiyo ni siku ya Nyerere (Nyerere day). Au siku ya ukimwi duniani, ikiangukia Jumamosi, je itawazuia wasabato wasifanye ibada siku hiyo, kwani ni siku ya ukimwi, hivyo wakifanya ibada zao watakuwa wanamwabudu mungu ukimwi? Ebu sasa turudi kwenye kuangalia majina ya siku zote saba kwa Kiingereza na maana yake;

>Jumatatu (Monday) - inatokana na moon day, kwa wapagani wa nyakati zile
                                      ilimaanisha siku  ya kumwabudu mungu moon (mwezi).
>Jumanne (Tuesday) –inatokana na tiw’s day, kwa wapagani wa nyakati zile
                                     ilimaanisha ni siku ya mungu Tiw.
>Jumatano (Wednesday) –inatokana na wedn day au woden day, kwa wapagani
                                     ilimaanisha siku ya mungu wedn au woden.
>Alhamisi (Thursday) –inatokana na thor day, kwa wapagani ilikuwa ni siku ya
                                     kumwabudu mungu thor.
>Ijumaa (Friday) - inatokana na frig day au freia day, kwa wapagani ilikuwa ni
                                     siku ya mungu frig au freia.
>Jumamosi (Saturday) –inatokana na Saturn day (siku ya sayari zohari), kwa
                                  wapagani ilikuwa ni siku ya kumwabudu mungu wa
                                 Kirumi aitwaye Saturn yaani kwa Kiswahili sayari ya zohari.
>Jumapili (Sunday) –ilitokana na sun day (siku ya jua), kwa wapagani wa
                                   Kirumi ilikuwa ni siku ya kumwabudu mungu sun (jua).

  Kwa ujumla, Siku zote za juma, Warumi walizipa majina ya miungu yao, kwa sababu hao kwa kipindi hicho ndiyo walikuwa watawala. Swali linakuja, kwa vile zimepewa majina ya miungu ya kipagani, hivyo siku zote hazifai kufanya ibada? Siku ya Jumamosi, Warumi walikuwa wakimwabudu mungu Saturn kwa Kiswahili zohari, swali ni kwamba, kwa kufanya ibada zao Jumamosi, wasabato wote wanamwabudu mungu zohari yaani sayari ya zohari (Saturn)?
  Mtoto wa Mungu ni lazima ufahamu kwamba, kupewa jina baya la siku, halikuzuii wewe siku hiyo kumwabudu Mungu wa kweli, kwa sababu jina hilo halitoki kwa Mungu bali hutoka kwa mwanamu ambaye hajawahi kuiumba siku. Kwa hiyo kama msabato atakwambia kuwa unafanya ibada Jumapili (Sunday) hivyo unamwabudu mungu jua, basi wewe utamjibu unafanya ibada Jumamosi (Saturday), hivyo unamwabudu mungu sayari ya Saturn (zohari). Hata hivyo wanaomwabudu Mungu wa kweli siku ya Jumapili, hawafanyi ibada kwa mungu jua, bali wanafanya ibada kwa Mungu wa kweli aliyeumba Jua.

3. Wasabato hudai kwamba, kwa vile Bwana Yesu aliingia hekaluni siku ya sabato (Marko 1:21; Luka 4:31), hivyo alishika sabato.

   Hoja hii pia si ya msingi na wala si ya kweli. Katika utafiti wangu nilioufanya, nimegundua kuwa waumini wa dhehebu la wasabato, asilimia 99 hawaelewi maana ya neno sabato, na hata walipoletewa dhehebu hili kutoka Marekani, walikuwa hawajatafuta kuchunguza maandiko kama watu wa Beroya (Matendo 17:11-12). Sabato maana yake ni pumziko la kazi, na kuingia hekaluni haina mahusino na neno sabato. Kuingia hekaluni siku ya kwanza ya juma (Jumapili) na siku ya saba kwa wana wa Israeli ilikuwa ni agizo la kusanyiko la kawaida (Kutoka 12:16). Ila kama Biblia ingesema Bwana Yesu alipumzika kufanya kazi siku ya sabato, hapo tungesema kuwa alishika sabato.
   Anayejua kuwa Bwana Yesu alishika sabato au la ni wasabato halisi (Mafarisayo) wa nyakati za Yesu, maana hao ndiyo waliopewa kushika sabato na Mungu mwenyewe, na siyo wanaojiita wasabato leo ambao wameagizwa kushika sabato na waanzilishi wa dhehebu hilo. Ebu tuwasikilize wasabato halisi (Mafarisayo) zama za Yesu wanasemaje, je Bwana Yesu alishika sabato au la? Katika kitabu cha Yohana 9:16 Biblia inasema, “Basi baadhi ya Mafarisayo wakasema, Mtu huyu hakutoka kwa Mungu, KWA SABABU HASHIKI SABATO. Wengine wakasema, awezaje mtu mwenye dhambi kufanya ishara kama hizo, kukawa matengano kati yao.” Unaona ukweli kutoka kwa wasabato halisi, wanakiri kabisa kwamba, Bwana Yesu hakushika sabato. Bwana Yesu siku ya sabato aliendelea kufanya shughuli zake kama kawaida, Yohana 5:16-18 Biblia inasema, “Basi kwa sababu hiyo Wayahudi walizidi kutaka kumwua, KWA KUWA HAKUIVUNJA SABATO TU, bali pamoja na hayo, alimwita Mungu Baba yake.” Oh Halleluya! Tunaona jinsi Bwana wetu alivyovunja sabato na ndiyo maana, wakataka kumwua. Kama kweli, katika Agano jipya tunashika sabato, mbona Bwana wetu aliivunja sabato, na Yeye ndiyo kiongozi mkuu wa wokovu wetu (Waebrania 2:10)? Sasa ndugu jiulize, unamfuata Musa au unamfuata Bwana Yesu aliyeivunja sabato? Kama unamfuata Musa hutafika mbinguni, kwani yeye mwenyewe alishasema habari za kumfuata Bwana Yesu na siyo yeye, Kumbukumbu 18:15, tunasoma, “Bwana, Mungu wako, atakuondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zake kama nilivyo mimi; msikilize yeye.” Lakini kama unamfuata Bwana YESU sabato ya nini? Aliivunjwa kwa kuwa alijua ni kivuli tu, ilikuwa ni ishara yake, sasa yeye aliye pumziko la kweli amekuja, sasa sabato ya nini? Kama unasema unamfuata Bwana Yesu, na wakati bado, hautaki kuivunja sabato (kivuli), kamwe hutaweza kuona wokovu halisi uliotokana na kazi ya msalaba. Kwa kuwa Yeye ndiye kiongozi wako na Mungu wako, na aliivunja sabato na wewe uivunje, kwa kuwa sisi sote tunamfuata Kristo kwa kila neno na tendo.

SABABU ZILIZOPELEKEA BWANA YESU KUINGIA HEKALUNI
SIKU YA SABATO

   Tukisoma katika kitabu cha Matendo 13:13-15 Biblia inasema, Kisha Paulo na wenziwe wakang’oa nanga wakasafiri kutoka pafo, wakafika Perge katika Pamfilia. Yohana akawaacha akarejea Yerusalemu. Lakini wao wakatoka Perge, wakapita kati ya nchi, wakafika Antiokia mji wa Pisidia, wakaingia katika sinagogi siku ya sabato, wakaketi. Kisha baada ya kusomwa torati na chuo cha manabii, wakuu wa sinagogi wakatuma mtu kwao, na kuwaambia, NDUGU, KAMA MKIWA NA NENO LA KUWAFAA WATU HAWA, LISEMENI.” Nyakati za Biblia, kulikuwa na utaratibu kwenye masinagogi kwamba, baada ya kusoma torati na chuo cha manabii, wakuu wa masinagogi, walikuwa wakikaribisha watu, waliokuwa na jambo jema la kuwaambia watu kwenye kusanyiko. Sasa, kwa wahubiri kama Bwana Yesu na Paulo, hii kwao ilikuwa ni nafasi yao ya pekee sana ya kuwahubiria Wayahudi habari njema za ufalme wa Mungu, kwani walikuwa wamepotea kwa kuendelea kushika sheria ya sabato na mapokeo mengine. Kwa hiyo, Bwana Yesu na Mhubiri kama Paulo walitumia nafasi hii, kuwafikishia Mafarisayo na Wayahudi wengine habari njema, kwa kuwa siku ya sabato, watu wengi walifika hekaluni.
  Kwa hiyo, Bwana Yesu na mitume kama Paulo, hawakwenda hekaluni kukusanyika kwa kusudi la kushika sabato au kushiriki kusanyiko, bali waliwafuata Wayahudi waliokuwa bado wamefungwa na mzigo wa sabato na mapokeo mengine. Na kwa kulithibitisha hilo, Bwana Yesu, alikuwa akienda hekaluni kila siku kufundisha, na siyo siku ya sabato tu. Luka 19:47 tunasoma, “Naye akawa akifundisha kila siku hekaluni. Lakini wakuu wa makuhani, na waandishi, na wakuu wa watu walikuwa wakitafuta njia ya kumwangamiza.” Luka 21:37 tunasoma, “Basi kila mchana, alikuwa akifundisha hekaluni, na usiku huenda kulala katika mlima uitwao wa Mizeituni.”  Pia katika Yohana 18:20 tunasoma, “Yesu akamjibu, Mimi nimesema na ulimwengu wazi wazi; siku zote nalifundisha katika sinagogi na katika hekalu, wakusanyikapo wayahudi wote; wala kwa siri mimi sikusema neno lolote.” Tunaona hapa, Bwana Yesu, anathibitisha kuwa alikuwa akienda kwenye sinagogi na hekalu kila siku ili kufundisha watu, kwani ilikuwa ni sehemu ambayo angeweza kuwapata Wayahudi, hivyo kumpa nafasi ya kufundisha kweli ya neno la Mungu.

 4. Hoja ya nne, wasabato hudai kwamba, sheria ya kushika sabato haijakomeshwa na inaendelea hata sasa kwani imeamriwa kuwa ni agano la milele kama Biblia inavyosema katika Kutoka 31:16, “Kwa ajili ya hayo wana wa Israeli wataishika sabato, kuiangalia sana hiyo sabato, katika vizazi vyao vyote, ni agano la milele.”

   Kabla hatujaingia kwa undani zaidi katika kutafuta ukweli wa hoja hii, ni vizuri, watu wakielewa maana ya neno MILELE kwa msingi wa maisha ya duniani. Neno MILELE, likitumika kwa matumizi ya kidunia haimaanishi isiyo na mwisho, kwa kuwa hakuna umilele kwenye maisha ya hapa duniani, bali humaanisha muda mrefu. Lakini neno MILELE, likitumika nje ya matumizi ya kidunia, mfano maisha baada ya kufa, hapo ndipo milele humaanisha “isiyo na mwisho”. Kwa ujumla, siyo kila palipoandikwa kwenye biblia MILELE, inamaanisha isiyo na mwisho. Kwa mfano, katika kitabu cha 1 Samweli 27:12 tunasoma, “Hivyo akishi akamsadiki Daudi, akasema, amewachukiza kabisa hao watu wake Israeli; kwa hiyo atakuwa mtumishi wangu hata milele” Tunaona hapa, Akishi anamtangaza Daudi kuwa ni mtumishi wake hata milele, lakini, ebu tujiulize, kama kila litumikapo neno milele, lina maana isiyo na mwisho, je Daudi aliendelea kuwa mtumishi wa Akishi? Je baadaye hakuwa Mfalme? Akishi hapa, alimaanisha kwamba, Daudi kuwa mtumishi wake kwa muda mrefu. Mfano mwingine ni pale Bath-sheba alisema, “Mfalme Daudi na aishi milele.” (1 Wafalme 1:31), Bath-sheba alijua kuwa mwanadamu hawezi kuishi duniani bila kuwa na mwisho, hivyo hapo alimaanisha Mfalme Daudi aishi kwa muda mrefu. Pia Kumbukumbu 15:17 imezungumzia mtumishi wa milele; hapa haimaanishi mtu anakuwa mtumishi kwa muda usiyo na mwisho bali kwa muda mrefu.
  Mungu alipotumia neno milele kwenye agano la kushika sabato, hakumaanisha isiyo na mwisho, bali alimaanisha ni agizo la muda mrefu mpaka wakati wa kuikomesha ulipofika. Na kama, alimaanisha milele ikiwa na maana ya isiyokoma, je hiyo sabato itashikwa mpaka mbinguni? Na mbinguni hakuna kuhesabu siku hata tukapata siku ya jumamosi. Pia kama ingekuwa milele ya isiyo koma, basi kulikuwa hakuna haja ya Bwana Yesu kuja duniani na kuleta agano jipya, na wala hakukuwa na haja ya Yeye kuwa kinyume na sabato, kama tulivyo kwisha kuona hapo nyuma. Bwana Yesu ni Mungu, Yeye ndiye aliyeiweka sabato iwe kama kitu cha kumwakilisha, alipokuwa kabla ya hajakuja duniani. Baada ya kuja alikuwa na mamlaka ya kuiondoa sawasawa na makusudi yake. Ni sawa tu na tunapotoa matangazo ya kuja kwa muhubiri fulani au muimbaji fulani, huwa tunaweka picha yake kwenye vipeperushi na matangazo, lakini muhubiri au muimbaji huyo akishafika, hatuendelei kuangalia picha zilizo kwenye vipeperushi na matangazo, bali tunatupa vyote na kwenda kumwona uso kwa uso.

5. Hoja nyingine kutoka kwa wasabato hujengwa katika kitabu cha Mathayo 5:17-18 inayosema, “Msidhani ya kuwa nalikuja kutangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, BALI KUTIMILIZA. Kwa maana, amini, nawaambia, mpaka mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati haitaondoka, hata yote yatimie.”
 
   Hoja inayojengwa na wasabato katika andiko hili, ni kwamba, Bwana Yesu anakiri hajakuja kutangua torati wala manabii bali amekuja kuitimiliza, yaani wakimaanisha kuwa, naye amekuja kuishika sabato. Watoto wa Mungu, hii hoja ni ya undanganyifu. Kuupata ukweli, ni vizuri turudi kwenye Biblia ya Kiingereza ya toleo la King James ili tupate tafsiri nzuri zaidi. Mathayo 5:17, “Do not think that I came to destroy the law or the prophets. I did not come to destroy but to FULFILL…..” Kadhalika na matoleo mengine ya Kiingereza, neno ‘Kutimiliza’ kwa Kiingereza limetumika ‘FULFILL’. Kulingana na kamusi ya Kiingereza, neno ‘fulfill’ lina maana zifuatazo; maana ya kwanza ya ‘fulfill’ ni ‘fill up’ yaani ‘jazia.’ Kwa hiyo inaleta maana ya kwamba, Bwana Yesu, hakuja kuitangua bali amekuja kuijazia (fill up), kwani kulikuwa kuna mapungufu katika lile agano. Na ndiyo maana katika kitabu cha Waebrania 8:7 tunasoma, “Maana kama lile la kwanza, lingalikuwa halina upungufu, nafasi isingalitafutwa kwa lile la pili.” Maana ya pili ya ‘fulfill’ ni ‘an act of doing something to satisfaction’ ikiwa na maana kwamba ni kitendo cha kufanya kitu ili kifike kwenye utoshelevu. Kwa hiyo, Bwana Yesu hakuja kuitangua torati na manabii, bali amekuja kuboresha ili ifikie utoshelevu, maana bado torati na manabii, haikuleta utoshelevu wala kuleta matokeo mazuri kwa watu, kwani kila kukicha watu walikuwa wakiuawa kwa kushindwa kuiishi torati. Maana ya tatu ya ‘fulfill’ ni ‘an act of achieving goal’ kwa Kiswahili inamaanisha ni kitendo cha kufanya kitu kifike kwenye malengo. Kwa hiyo kwa lugha nyingine tungeweza kusema kwamba, Bwana Yesu amekuja kuifanya torati na manabii iweze kufikia malengo aliyokusudia, kwa sababu bado ilikuwa na shida kulingana na uwezo wa mwanadamu. Sasa kwa lugha fasaha ni kwamba, Bwana Yesu, hakuja kuiondoa torati na manabii, bali alikuja kufanya maboresho, marekebisho, masahihisho; ikiwa na maana kwamba kilichotakiwa kuondoka kiliondoka, na kilichotakiwa kubaki, kilibaki; na hii ilifanya na chekecho la msalaba. Mfano, mambo ya kushika sabato yaliondolewa, kwa sababu sabato ilikuwa ni amri ya ishara, ilikuwa ni kivuli, ikimuashira Yeye Bwana Yesu mwenyewe kama pumziko la kweli la kiroho. Hivyo, kwa vile Yeye pumziko halisi amekuja, sabato haikuwa na kazi tena. Bwana Yesu anasema, “Njooni kwangu, ninyi nyote msumbukao, na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.”(Mathayo 11:28)
  Upungufu wa Agano la lake unaozungumziwa katika Waebrania 8:7, haupo katika torati, kwani torati kwa asili, haina tatizo na ni njema maana ni maagizo ya Mungu mwenyewe. Tatizo lilikuwa kwenye uwezo wa wanadamu wenyewe katika kuifuata torati yote kwa nguvu zao; maana kipindi cha agano la kale, walipewa sheria na hukumu tu, lakini hawakuwa na neema ya kuwafanya washike hiyo sheria. Kwa hiyo, kimsingi wana wa Israeli waliipenda torati (sheria) na hukumu walizopewa na Mungu, na waliikubali hiyo torati (sheria) na hukumu, na ndiyo maana walikubali kufanya agano na Mungu, kwa kuwa kila agano ni lazima kuwepo kwa makubaliano katika pande mbili.
  Mioyoni mwao waliikubali na kuipenda torati (sheria) na hukumu zake, lakini mwili uliwazuia kuitekeleza hiyo torati, kwa kuwa walipewa torati (sheria) na hukumu tu bila neema au kiwezesho cha kuiishi sheria. Sasa hapo ndipo tunapopata upungufu wa Agano la kale. Katika kitabu cha Warumi 7:14-16 tunasoma, “Kwa maana twajua kuwa torati asili yake ni ya rohoni; bali mimi ni mtu wa mwilini, nimeuzwa chini ya dhambi. Maana sijui nifanyalo; kwa sababu lile nilipendalo, silitendi; bali lile nilichukialo ndilo ninalolitenda.Lakini kama nikilitenda lile nisilolipenda, naikiri ile sheria ya kuwa ni njema. Basi sasa si mimi nafsi yangu ninayetenda hilo, bali ni ile dhambi ikaayo ndani yangu. Kwa maana najua ya kuwa ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai neno jema; kwa kuwa kutaka nataka, bali kutenda lililo jema sipati.” Kama nilivyo kwisha kusema hapo nyuma kwamba, wana wa Israeli waliipenda torati na hukumu. Lakini katika viungo vya mwili yaani utu wa nje, sheria ilikuwa ni kama ni mzigo mzito sana; kwa sababu kwa asili, ndani ya mtu halikai neno jema. Na kwa sababu hiyo, wana wa Israeli hawakuweza kudumu katika Agano la kale kama maandiko yanavyotuambia katika, Waebrania 8:9, “Halitakuwa kama agano lile nililoagana na baba zao, katika siku ile nilipowashika mikono yao niwatoe katika nchi ya Misri. KWA SABABU HAWAKUDUMU KATIKA AGANO LANGU, mimi nami sikuwajali, asema Bwana.” Pia katika kitabu cha Ezekieli 20:21 Biblia inasema, “Lakini watoto hao waliniasi; hawakuenda katika amri zangu, wala hawakuzishika hukumu zangu kuzitenda, ambazo mwanadamu ataishi kwazo kama akizitenda; walizitia unajisi sabato zangu; ndipo nikasema, kwamba nitamwaga ghadhabu yangu juu yao, ili kuitimiza hasira yangu juu yao jangwani.”
   Kwa ujumla ukisoma vitabu vyote vya Musa, utagundua kwamba wana wa Israeli hawakukaa vizuri kwenye sheria na hukumu za lile agano. Ndipo Mungu kwa huruma yake akaleta Agano lingine, lililo bora zaidi kuliko lile la kwanza, na mdhamini wa Agano hili ni Mungu mwenyewe, wakati Mdhamini wa agano la kale alikuwa mwanadmu (Musa). Waebrania 7:22 tunasoma, “Basi kwa kadiri hii Yesu amekuwa mdhamini wa agano lililo bora zaidi.”
   Hivyo basi, ni neno la kuaminiwa, tena lastahili kukubalika, kuwa mweka sheria katika Agano la kale, amekuja kurekebisha sheria na kufanya Agano upya, hivyo lile la kwanza kutotenda kazi; Waebrania 8:13 tunasoma, “Kwa kule kusema, Agano jipya, amelifanya lile la kwanza kuwa kuukuu. Lakini kitu kianzacho kuwa kikuukuu na kuchakaa ki karibu na kutoweka.”

6. Katika hoja ya sita, baadhi ya wasabato hudai kwamba hakuna kuokoka duniani na wala hakuna watakatifu, na wanasimamia hoja hiyo katika maandiko yafuatayo; Mhubiri 7:20; Warumi 3: 12, 23; Warumi 5:12; Zaburi 14:3.
   Kabla hatujaingia kwa undani zaidi, si vibaya kama tutafahamu maana ya neno kuokoka kama linavyotumiwa na watoto wa Mungu. Kuokoka maana yake ni kusalimika kutoka katika hatari iliyo dhahiri. Kwa mfano, mtu aliyesalimika kufa kwenye ajali ya gari, mtu huyo tunasema ameokoka na ajali ya gari. Kuokoka katika dhana ya Kiroho, haina tofauti sana na maana tuliyoizungumzia hapo nyuma, lakini utofauti wake upo kwenye aina ya hatari. Mtu ambaye hajamwamini na kumkiri Bwana Yesu, ni wazi kabisa yupo katika hatari ya kwenda kwenye hukumu ya mateso ya moto wa milele, kama maandiko yanavyotuambia katika Yohana 3:18; Yohana 5:22. Lakini kwa mtu ambaye amemwamini Mwana wa Mungu, huyo haukumiwi, kwa maana hiyo, mtu huyo anakuwa ameokoka au amesalimika na hatari ya kwenda kwenye mateso ya moto wa milele; Yohana 3:18 tunasoma, “Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.” Marko 16:16 Maandiko yanasema, “Aaminiye na kubatizwa ATAOKOKA; asiyeamini atahukumiwa.Waefeso 2:5 Maandiko yanakiri kwamba tumeokolewa kwa neema. Kadhalika maandiko katika Isaya 45:20 tunasoma, “Jikusanyeni mje; na kukaribia pamoja, ninyi wa MATAIFA MLIOOKOKA…..”  
  Jambo la msingi ambalo watu wanapaswa kufahamu ni kwamba, baba yetu Adamu alipofanya dhambi, na sisi wanadamu wote, tukahesabiwa kuwa tuna dhambi kama maandiko yanavyosema katika Warumi 5:12. Kwa hiyo, kama kwa kuasi kwake baba yetu Adamu, na sisi sote tukaingizwa katika hali ya wenye dhambi, basi kwa kutii kwake mmoja ambaye Bwana wetu Yesu Kristo, na sisi tunaomwamini tumeingizwa katika hali ya wenye haki yaani utakatifu (Warumi 5:19). Adamu alipokosea na sisi tukawa tumekosea, Bwana Yesu alipopatia na sisi tukawa tumepatia. Kwa hiyo ni dhahiri kabisa kuokoka ni hapa duniani, na wakamilifu wapo duniani, na Zaburi 16:3 maandiko yanasema, “Watakatifu waliopo duniani ndiyo walio bora, hao ndio niliopendezwa nao.”  Paulo anawaita wenzake watakatifu, 2 Wakorintho 13:13 tunasoma, “Watakatifu wote wawasalimu.”  Paulo pia anathibitisha kuwepo kwa watakatifu duniani katika Wafilipi 4:21-22 tunasoma, “Msalimieni kila MTAKATIFU katika Kristo Yesu. Ndugu walio pamoja nami wawasalimu. WATAKATIFU wote wawasalimu, hasa wao walio wa nyumbani mwa Kaisari.”
Mungu mwenyewe anamthibitisha Ayubu kuwa alikuwa mkamilifu (Ayubu 1:8). Maandiko yanatuthibitishia kuwa Nuhu pia alikuwa mtu wa haki na mkamilifu (Mwanzo 6:9). Watoto wa Mungu, ukamilifu tunaupata hapa hapa duniani na siyo mbinguni, na ndiyo maana Bwana Yesu anasema katika Mathayo 5:48, “Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Soma pia Waebrania 12:14, Walawi 19:2).


KUSHIKA SIKU YA SABATO KUNAAMBANA NA TORATI YOTE YA MUSA

   Maandiko, katika kitabu cha Yohana 1:17 yanasema, “Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo.” Watoto wa Mungu, ni jambo la msingi sana kufahamu kwamba, tunapotaja neno torati, tunamaanisha Amri kumi, sheria 613 na hukumu zake.

TORATI = AMRI KUMI + SHERIA 613 + HUKUMU ZAKE

   Kwa nyakati za agano la kale, ilikuwa, huwezi kuwa mkamilifu kwa kushika amri kumi tu bila kushika na sheria nyingine 613 na kuzitendea kazi hukumu zake. Mtu asiyetendea kazi yote yaliyoandikwa katika torati, alikuwa amelaaniwa; Galatia 3:10 tunasoma, “Kwa maana wale wote walio wa matendo ya sheria, wako chini ya laana; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu asiyedumu katika YOTE yaliyoandikwa katika kitabu cha torati, ayafanye.”  Mungu aliwaagiza wana wa Israeli washike torati yote; Walawi 20:22 tunasoma, “Basi zishikeni amri zangu ZOTE, na hukumu zangu zote, na kuzifanya; ili kwamba hiyo nchi, ambayo nawapeleka ninyi kuiketi isiwatapike.”  Pia Kitabu cha Kutoka 35:10 Biblia inasema, “Na kila mtu kati yenu aliye na moyo wa hekima na aje, na kuyafanya haya YOTE ambayo Bwana ameagiza.” Kwa mtu anayeng’ang’ania sheria ya kushika sabato na makatazo ya baadhi ya vyakula katika nyakati hizi za Agano jipya, mtu huyo ni wazi kabisa, hayupo kwenye fungamano la Agano Jipya, maana tumeona bayana kwamba, sheria hii, Bwana hakuipitisha, kwa kuwa ilikuwa ni ishara, iliyokuwa ikimuashiria Yeye kama (sabato) pumziko la kweli la kiroho (Wakolosai 2:16-17). Hivyo kushika sabato ni kukataa sheria ya Kristo na kuikubali sheria ya Musa. Na sharti la sheria ya Musa (torati) ni kwamba, ni lazima mtu ashike Amri kumi zote, sheria nyingine 613 na hukumu zake. Mfano; sheria ya kushika sabato ilikuwa na hukumu yake, pale ambapo mtu, alionekana kutoitimiza, yaani alipaswa kuuawa; Kutoka 31:14 tunasoma, “Basi mtaishika hiyo sabato; kwa kuwa ni takatifu kwenu; kila mtu atakayeitia unajisi hakika yake atauawa, kwa kuwa kila mtu afanyaye kazi katika siku hiyo, nafsi hiyo itakatiliwa mbali na watu wake.” Kitabu cha Kutoka 35:2 Biblia inasema, “Fanyeni kazi siku sita, lakini siku ya saba itakuwa siku takatifu kwenu; ni sabato ya kustarehe kabisa kwa Bwana; mtu awaye yote atakayefanya kazi yoyote katika siku hiyo ATAUAWA.”
   Kama Mungu alitoa agizo la kushika sabato, na pia akatoa agizo kuwa atakayefanya kazi yoyote siku hiyo ni lazima auawe; Je ni wasabato wangapi leo tunawaona wanafanya kazi Jumamosi, kama kuna usahihi wowote mbona hatuoni wakiitekeleza hukumu ya kuuana? maana ni agizo la Mungu mwenyewe. Yakobo 2:10 inasema mtu akiishika sheria yote, akajikwaa katika neno moja tu, amekosa juu ya yote. Wapendwa! hii ndiyo sababu iliyompelekea Bwana Yesu kuivunja sabato, baadhi ya sheria na hukumu zote; kwa kuwa ilikuwa ni huduma ya mauti (2 Wakorintho 3:7). Mtu anayeshika sheria ya sabato katika nyakati hizi za agano jipya, anapaswa kushika na amri tisa zote, pamoja na sheria 613 na hukumu zake, ambazo zote zimefafanuliwa kwenye vitabu vya Kutoka, Mambo ya Walawi, Hesabu na Kumbukumbu la torati. Lakini kama Wayahudi walishindwa, sisi tutaweza wapi? Watoto wa Mungu, tusikubali kujitwisha mizigo ambayo Bwana wetu alikwisha itua, kwa nini tuendelee kukaa kwenye makosa yaliyofanyika katika agano la kwanza; Waebrania 9:15 tunasoma, “Kwa sababu hii ni mjumbe wa agano jipya,ili, mauti ikiisha kufanyika, KWA KUKOMBOA MAKOSA YALIYOKUWA CHINI YA AGANO LA KWANZA, hao walioitwa waipokee ahadi ya urithi wa milele.” Kazi ya torati (ikiwemo sheria ya sabato) ilikuwa ni kama kiongozi cha kutuleta kwa Bwana Yesu kama maandiko yanavyosema katika kitabu cha Wagalatia 3:24-26 tunasoma, “Hivyo torati imekuwa kiongozi kutuleta kwa Kristo, ili tuhesabiwe haki kwa imani. Lakini, iwapo imani imekuja, hatumo tena chini ya kiongozi (torati-ikiwemo sabato).” Sabato ni kama kiongozi cha kutuleta kwa Kristo maana Yeye ndiye sabato mwenyewe (pumziko), sasa kwa vile Kristo amekuja, sasa hatupasWi kuing’ang’anisa sabato.

MADHARA YA KUSHIKA SHERIA YA SABATO
1. Kushika sabato kuna mfanya mtu asiwe mwana funzi wa Yesu, bali mwanafunzi wa Musa, kwa kuwa torati ilikuja kwa mkono wa Musa na neema na kweli vilitolewa kwa mkono wa Yesu (Yohana 1:17).
2. Kushika siku ya sabato ni mafundisho manyonge na yenye upungufu, hivyo kumfanya mtu awe mwana wa Jehanamu mara mbili (Mathayo 23:15). Kitabu cha Wagalatia 4:9-10 Biblia inasema, “Bali sasa mkiisha kumjua Mungu, au zaidi kujulikana na Mungu, kwa nini kuyarejea tena mafundisho ya kwanza yaliyo manyonge, yenye upungufu, ambayo mnataka kuyatumikia tena? MNASHIKA SIKU, na miezi, na nyakati, na miaka.
3. Kushika sabato, kunamfanya mtu kuwa chini ya laana. Na hii ni kwa sababu sabato ni sheria iliyo katika torati; na tunaposema torati, tunamaanisha amri kumi, sheria 613 na hukumu zake. Na ilikwisha kuandikwa kuwa mtu asiyeshika torati yote ni amelaaniwa; Galatia 3:10 tunasoma, “Kwa maana wale wote walio wa matendo ya sheria, wako chini ya laana; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu asiyedumu katika YOTE yaliyoandikwa katika kitabu cha torati, ayafanye.”  Kristo ndiye aliyetukomboa kutoka katika laana ya torati (Wagalatia 3:13), na ndiyo maana ukimwamini Bwana YESU, ni lazima ufuate sheria ya Kristo (Wagalatia 6:2), na siyo sheria ya Musa. Kushika sabato (pumziko) siyo sheria ya Kristo, na Bwana Yesu na Baba yake waliipinga kama tunavyoweza kusoma katika Yohana 5:16-18, “Kwa sababu hiyo Wayahudi wakamwuudhi Yesu, kwa kuwa alitenda hayo siku ya sabato. AKAWAJIBU, BABA YANGU ANATENDA KAZI HATA SASA, NAMI NINATENDA KAZI. Basi kwa sababu hiyo Wayahudi walizidi kutaka kumwua, kwa kuwa HAKUIVUNJA SABATO TU, bali pamoja na hayo, alimwita Mungu Baba yake, akijifanya sawa na Mungu.” Swali ni hili, huyu Yesu liyeshika sabato na kuwafundisha watu leo washike sabato ni Yesu yupi?
3. Kushika sabato kuna mfanya mtu awe mwilini; na mtu anayeufuata mwili ni ngumu sana kumpendeza Mungu (Warumi 8:8), kwa kuwa hatoweza kushinda dhambi. Na ndiyo maana utaona mtu anashika sabato, lakini bado haogopi kwenda kwa waganga wa kienyeji, haoni ni makosa kubishana, haoni dhambi kufanya uasherati na uzinzi. Kwake kuinadi sabato ndiyo injili, kuliko kumnadi Bwana Yesu.
4. Kushika sabato kunatengeneza ngome ya kifarisayo ndani ya mtu; na madhara ya ngome hii ni kwamba, hata kama mtu akisikia ukweli kutoka kwa Mungu mwenyewe, bado mtu huyo hawezi kuusikia wala kuufuata ukweli huo. Ufahamu wa mtu unafungwa hata nuru ya wokovu isimzukie (2 Wakorintho 4:4), hivyo moja kwa moja mtu anakuwa amekata tiketi ya kwenda Jehanam ya moto.
5. Kushika sabato kunamfanya mtu awe mnafiki. Mtu mnafiki huwa na kawaida ya kutangaza sheria na kuitilia mkazo, lakini yeye mwenyewe haitendei kazi. Luka 13:15 Biblia inasema, “Lakini Bwana akamjibu akasema, Enyi wanafiki, kila mmoja wenu, je! Hamfungui ng’ombe wake au punda wake siku ya sabato katika zizi, aende naye kumnywesha?”  Na ukweli ni kwamba hakuna mnafiki atakayeurithi ufalme wa Mungu.

KUKOMESHWA KWA SABATO
   Agizo la kushika siku ya sabato na torati yote kwa ujumla, ilikuwa ni huduma ya mauti au huduma ya adhabu ya kifo; Katika kitabu cha 2 Wakorintho 3:7-8 tunasoma, “Basi, ikiwa huduma ya mauti iliyoandikwa na kuchorwa katika mawe, ilikuja katika utukufu, hata Waisraeli hawakuweza kuukazia macho uso wa Musa, kwa sababu ya utukufu wa uso wake; nao ni utukufu uliokuwa ukibatilika. Je huduma ya roho haitazidi kuwa katika utukufu?” Kwa hiyo torati yote ikiwemo kushika sabato, ilikuwa ni huduma ya mauti. Pia torati haikuwa huduma ya mauti tu, bali ilikuwa ni nguvu za dhambi, kama maandiko yanavyosema katika kitabu cha 1 Wakorintho 15:56, “Uchungu wa mauti ni dhambi, na nguvu za dhambi ni torati.” Kwa kadiri unavyozidi kuifuata torati ndivyo nguvu ya dhambi inavyozidi, kwa kuwa torati kazi yake ni kubaini makosa. Haina tofauti na darubini ya kupima vijidudu vya magonjwa. Kwa vile torati ilikwisha tolewa katika agano la kale na imetufanya kujua dhambi nini; hivyo katika agano jipya, haupaswi tena kuifuata torati, bali tunapaswa kuifuata dawa ya dhambi, ambayo ni Bwana wetu Yesu Kristu. Warumi 8:2 Biblia inasema, “Kwa sababu sheria ya Roho ya uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya dhambi na mauti.”
  Kwa ujumla ni kwamba, torati ilikuwa ni huduma ya mauti, kwa kuwa sheria walizoshindwa kuzifuata Wana wa Israeli, iliwalazimu kuuawa. Watu wengi walikufa kwa nguvu ya torati; mfano mtu ambaye hakushika sabato aliuawa (Kutoka 31:14-15; Kutoka 35:2-3). Mtu aliye jaribu kukusanya kuni siku ya sabato kwa kusudi la kujipikia chakula aliuawa (Hesabu 15:32-36). Watu wagonjwa hawakutakiwa kutibiwa siku ya sabato hivyo kusababisha watu wengi kufa (Luka 13:14), kitu ambacho si mpango wa Mungu.
  Hata hivyo, pamoja na torati kuwa ni huduma ya mauti, pia Wana wa Israeli wenyewe, hawakuweza kudumu katika lile agano la kwanza walilofanya na Mungu, hivyo kufanya agano hilo, kutofanikiwa; Yohana 7:19 tunasoma, “Je! Musa hakuwapa torati? Wala hakuna mmoja wenu aitendaye torati.” Ni vema ifahamike kuwa, kinachofanya agano kudumu, ni kutimizwa kwa masharti au sheria au taratibu za agano husika. Katika agano lolote au mkataba wowote ule, ni lazima kuwepo kwa masharti au sheria zilizowekwa, ili kuulinda mkataba au agano hilo. Kwa hiyo mtu anayevunja sheria katika mkataba au agano fulani, tayari yeye, ndiye anayekuwa amevunja huo mkataba au hilo agano. Wana wa Israeli walifanya agano na Mungu, na agano hilo lililindwa na vifungu vya sheria ambavyo ni torati yote; sasa kwa vile wote walikosa kuitendea kazi torati kama tunavyoona katika Yohana 7:19; Ezekieli 20:21, hivyo, kitendo cha kutoitendea kazi torati, tayari walikwisha vunja agano la kwanza na siyo Mungu. Na ndiyo maana zama za Nabii Isaya, Bwana alimtumia Nabii huyo kuwaambia wana wa Israeli kwamba yeye hataki tena sabato zao na ibada zao; Isaya 1:13 tunasoma, “Msilete tena matoleo ya ubatili; uvumba ni chukizo kwangu; mwezi mpya na SABATO, kuita makutano; siyawezi maovu hayo na makutano ya ibada.”
   Vitu hivi vyote, havikuwa na maana tena mbele za Mungu kwa kuwa tayari wana wa Israeli walikwisha liharibu Agano Lake. Na kama agano lilikwisha haribika, kushika sabato na ibada zao zilikuwa na maana gani mbele za Mungu? Hivyo kwa huruma yake, aliamua kufanya mpango mpya wa kuweka agano jipya na sheria zikiwa zimeboreshwa.
   Kabla ya kukomeshwa kwa sabato na agano la kwanza kwa ujumla, Mungu kwa hekima yake alianza kuwatumia manabii kutoa matangazo juu ya ujio wa agano jipya na kukomeshwa sabato;
1.      Nabii Hosea alitoa unabii juu ya kukomeshwa kwa sabato na siku za kusanyiko zilizoamriwa. Hosea 2:11 tunasoma, “Tena nitaikomesha furaha yake yote, na sikukuu zake, na siku zake za mwandamo wa mwezi, NA SABATO ZAKE, na makusanyiko yake yote yalioamriwa.”
2.      Baada ya kutofanikiwa kwa torati, Musa alitangaza kabisa ujio wa mdhamini wa agano jipya (Bwana Yesu) na ujio wa sheria ya Kristo. (Kumbukumbu 18:15-19).
3.      Nabii Isaya alianza kupiga debe juu ya ujio wa agano jipya (Isaya 55:3).
4.      Yeremia naye hakubaki nyuma, naye alianza kupiga mbiu juu ya agano jipya (Yeremia 31:31; 32:40).

SABABU ZA NYONGEZA ZA KUKOMESHWA KWA SABATO NA TORATI YOTE KWA UJUMLA
1.      Torati ilikuwa ni kivuli tu cha mema yatakayo kuja na haikuwa kitu halisi. Waebrania 10:1 tunasoma, “Basi torati, kwa kuwa ni kivuli cha mema yatakayokuja, wala si sura yenyewe ya mambo hayo, kwa dhabihu zile zile wanazozitoa kila mwaka daima, haiwezi wakati wowote kuwakamilisha wakaribiao.” Sabato ni sehemu ya torati, hivyo wanaoshika sabato, ni vema waelewe kuwa, sabato si kitu halisi, ilikuwa ni kivuli tu.
2.      Torati ni kiongozi tu cha kutuleta kwa Yesu. Wagalatia 3:24-26 tunasoma, “Hivyo torati imekuwa kiongozi kutuleta kwa Kristo, ili tuhesabiwe haki kwa imani. Lakini iwapo imani imekuja, hatupo tena chini ya kiongozi.” Mfano; Wewe ni mgeni, na umefika maeneo ambayo unataka kukutana na mwenyeji wako, na wakati huo huo, ukakutana na mtu usiyemjua, na kwa baati nzuri huyo mtu, akasema kuwa mwenyeji wako unayemtafuta, ninafahamu alipo, hivyo, akaamua kukupeleka. Baaada ya huyo mtu kukufikisha, je utaamua kumng’ang’ania huyo aliyekupeleka au utabaki na mwenyeji wako, uliyekusudia kufika kwake. Sasa sabato ilikuwa ni kiongozi cha kutupeleka kwa Kristo, sasa kwa sababu tumempata Kristo, hatuhitaji tena sabato.
3.      Torati ilikuwa haiondoi uhitaji yaani ilikuwa haitibu dhambi bali ilikuwa ikibaini dhambi na kuadhibu. 2 Wakorintho 3:15-16 tunasoma, “Ila hata leo, torati ya Musa isomwapo, utaji huikalia mioyo yao. Lakini wakati wowote watakapomgeukia Bwana, ule utaji huondolewa.
4.      Kuwa chini ya torati ni kuwa chini ya laana, kwa sababu ilimlazimu mtu kuifuata torati yote bila kuacha hata kitu kimoja. Hii haikuwezekana, hivyo kuwafanya watu wote kuwa chini ya laana (Wagalatia 3:10; 5:3-4).
5.      Torati huchochea nguvu ya dhambi (1 Wakorintho 15:56).

ANGALIZO
1.      Torati (ikiwemo na sheria ya kushika sabato) pamoja na manabii, vilikuwapo mpaka Yohana mbatizaji; Luka 16:16 Biblia inasema, “Torati na manabii vilikuwapo mpaka Yohana; tangu wakati huo habari njema ya ufalme wa Mungu, hutangazwa, na kila mtu hujiingiza kwa nguvu.” Kwa hiyo, kushika sabato ilikuwa mwisho wake nyakati za Yohana Mbatizaji na siyo nyakati hizi za Agano jipya.
2.      Watu waliompokea Bwana Yesu kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yao, hao ni wahudumu wa Agano jipya; 2 Wakorintho 3:6, tunasoma, “Naye ndiye aliyetutosheleza, kuwa wahudumu wa Agano jipya; si wa andiko, bali wa Roho, kwa maana andiko huua, bali Roho huhuisha.”
3.      Katika nyakati hizi za Agano jipya, hatuifuati torati bali tunaifuata sheria ya Kristo (Wagalatia 6:2). Wagalatia 5:14 tunasoma, “Maana torati yote imetimilika katika neno moja, nalo ni hili, umpende jirani yako kama nafsi yako.” Kitabu cha Mathayo 22:37-40 tunasoma, “Akamwambia, mpende Bwana Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, mpende jirani yako kama nafsi yako. Katika amri hizi, hutegemea torati yote na manabii.” Hizi zote ni miongoni mwa sheria ya Kristo; Wagalatia 6:2 inasema, “Mchukuliane mizigo na kuitimizwa hivyo sheria ya Kristo.”
4.      Bwana YESU alifanya kazi siku ya sabato (Yohana 5:16-18; Yohana 9:16), lakini bado Biblia inasema hakufanya dhambi (Waebrania 4:15). Kushika sabato nyakati za leo ni maagizo ya waanzilishi wa dhehebu hilo na siyo maagizo ya Bwana YESU (Waanzilishi hao ni William Miller 1782-1849; Hiram Edson; Joseph Bates na Hellen Gould White).
5.      Mpendwa mtoto wa Mungu, kushika sabato katika Agano jipya si maagizo ya Mungu, kamwe usikubali kuifuata, maana utatolewa kutoka katika uanafunzi wa Yesu na kuwa mwanafunzi wa Musa. Na isitoshe neno la Mungu katika Wakolosai 2:16 linasema, “Mtu asiwahukumu ninyi katika vyakula au vinywaji, au kwa sababu ya sikukuu au mwandamo wa mwezi, au SABATO. Mambo hayo ni kivuli cha mambo yajayo; bali mwili ni wa Kristo.” Mtu akikwambia kuhusu kushika sabato au sheria za kutokula vyakula na kunywa vinywaji, mwambie, “Siwezi kushika kivuli, maana Biblia inasema hayo yote yalikuwa ni kivuli cha mambo yajayo, bali ninamshika Kristo.”
6.      Anayeitegemea torati (ikiwemo na sabato), huyo ni kiongozi kipofu, mkufunzi wa wajinga na mwalimu wa watoto wachanga. Warumi 2:17-20 tunasoma, “Lakini wewe ukiwa unaitwa Myahudi na kuitegemea torati, na kujisifu katika Mungu, na kuyajua mapenzi yake, na kuyakubali mambo yaliyo bora, nawe umeelimishwa katika torati, na kujua hakika ya kuwa wewe mweyewe u kiongozi wa vipofu, mwanga wao walio gizani, mkufunzi wa wajinga, mwalimu wa watoto wachanga, mwenye namna ya maarifa na ya kweli katika torati.”
                             
SABABU ZINAZOWAPELEKEA WAKRISTO KUFANYA JUMAPLI KUWA SIKU YAO YA KUSANYIKO KUU LA IBADA.
  Kwa kipindi kirefu kumekuwapo na migogoro kwa Wakristo kuhusu siku halali ya kufanya ibada. Wakristo wanaoshika sheria ya siku ya sabato wamekuwa wakidai kuwa siku halali ya kufanya ibada ni Jumamosi, kadhalika na Wakristo wanaofanya ibada zao siku ya Jumapili husema kuwa siku halali ya kufanya ibada ni siku ya Jumapili. Kama majadiliano haya yangefanywa kwa msingi wa kimaadiko, basi nina amini kabisa kwamba, kamwe kusingekuwa na mgogolo wowote, kwa kuwa Neno la Mungu liko wazi kabisa. Ni vema ifahamike kwamba, Mungu wetu anapenda sana kuona watoto wake wakimwadudu kila siku na kila saa, na wala siyo katika siku fulani au masaa fulani. Matendo 26:7 Biblia inasema, “Ambayo kabila zenu kumi na mbili wanataraji kuifikia, wakimwabudu Mungu kwa bidii mchana na usiku……
      Lakini kwa vile sisi ni wanadamu, na tunahitaji kufanya shughuli za kutupatia mkate wa kila siku, hatuwezi kufanya kusanyiko la kumwabudu Mungu kila saa, hivyo hatuna budi kuwa na siku maalumu za makusanyiko. Bwana Yesu, kupitia Mutme Paulo amefundisha wazi wazi kuhusu siku za kufanya makusanyiko; Warumi 14:5-6, Biblia inasema, “Mtu mmoja afanya tofauti kati ya siku na siku, mwingine aona siku zote kuwa sawasawa. Kila mtu na athibitke katika akili zake mwenyewe. Yeye aadhimishaye siku, huiadhimisha kwa Bwana; naye alaye hula kwa Bwana…….” Swala la siku ipi watu wafanye kusanyiko, lipo chini ya maamuzi ya watu husika, kwa kuwa siku zote ni sawa, wanaweza wakachagua siku fulani na wakawa wanafanya makusanyiko, kwa kuwa kila aadhimishaye siku huiadhimisha kwa Bwana. Kama watu wataamua kufanya makusanyiko kila siku bado ni jambo jema.
   Utaratibu wa kufanya makusanyiko ya ibada siku ya Jumapili haukuanzishwa na Mfalme Constantine kama wanavyodai baadhi ya watu. Kabla ya Mfalme Constantine, Mitume katika kanisa la kwanza walikuwa wakikusanyika siku ya Jumapili; 1 Wakorintho 16:1-2 tunasoma, “Kwa habari ya ile changizo kwa ajili ya watakatifu, kama vile nilivyoamuru makanisa ya Galatia, nanyi fanyeni vivyo. Siku ya kwanza ya juma kila mtu kwenu na aweke akiba kwake; kwa kadiri ya kufanikiwa kwake; ili kwamba michango isifanyike hapo nitakapo kuja.” Pia Matendo 20:7-12 tunasoma, “Hata siku ya kwanza ya juma, tulipokuwa tumekutana kuumega mkate…..” Kwa hiyo, watoto wa Mungu wanaweza wakamwabudu Mungu katika siku zote saba, kwani Mungu hatazami siku, bali anawatafuta waabuduo halisi, ambao wanamwabudu Baba katika Roho na pia katika Kweli (Yohana 4:23-24).

SABABU ZA MSINGI ZINAZOWAPELEKEA WAKRISTO KUFANYA JUMAPILI KUWA SIKU YAO KUU YA KUSANYIKO LA IBADA
1. Mungu alikwisha iweka katika Agano la kale siku ya Jumapili kama siku ya kusanyiko ikiwa kama kiashirio cha siku ya matumaini kwa Wafuasi wa Kristo, kwani siku hii ndiyo Bwana alifufuka; Kutoka 12:16 tunasoma, “Siku ya kwanza kwenu kutakuwa na kusanyiko takatifu, na siku ya saba kutakuwa na kusanyiko takatifu…” Kwa hiyo agizo la kukusanyika siku ya Jumapili lilianza tangu Agano la kale kama kiashirio na kuthibitika katika Agano jipya.
2. Jumapili ni sikukuu ya malimbuko au mazao ya kwanza ambayo ilifanywa katika Agano la Kale, siku ya pili baada ya sabato (on the morrow after the Sabbath) (Walawi 23:9-14), ambayo ilifanywa kama kivuli cha sikukuu ya kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye ndiye limbuko lao waliolala mauti, mzaliwa wa kwanza katika wafu (1 Wakorintho 15:20; Wakolosai 1:18).
3. Jumapili ni siku ya ushindi wa Bwana wetu Yesu Kristo dhidi ya kifo na mauti. Alifufuka siku hiyo na kujidhihirisha kwa wanafunzi wake. Wokovu wetu unahusiana moja kwa moja na kufufuka kwa Yesu Kristo. Kufa na kufufuka ndiko kunakomtofautisha Bwana Yesu na manabii wengine. Yohana 20:1 tunasoma, “Hata siku ya kwanza ya juma Mariam Magdalene alikwenda kaburini alfajili, kungali giza bado; akaliona lile jiwe limeondolewa kaburini.”  Baada ya kufufuka siku ya kwanza ya juma ambayo ndiyo Jumapili, Bwana Yesu alikuwa akiwatokea wanafunzi wake siku ya kwanza ya juma, kuashiria kuwa hiyo ni siku ya matumaini wa wanafunzi wa Yesu (Yohana 1:19, 26). Kwa wanafunzi wa Yesu, siku ya Jumamosi haikuwa siku ya matumaini kwa kuwa siku hiyo bado Bwana alikuwa kaburini, na shetani na malaika zake bado walikuwa wakitamba siku hiyo. Kwa hiyo Jumapili ina maana kubwa sana kiroho kwa wanafunzi halisi wa Yesu.
4. Jumapili ndiyo siku aliyokuja duniani kiongozi mkuu wa kazi yote ya Mungu katika Kanisa yaani ROHO MTAKATIFU. Na huyu ndiye Bwana wa mavuno anayewapeleka watenda kazi shambani mwa Bwana. Roho Mtakatifu alikuja sawa sawa na ahadi ya Kristo, siku ya pentekoste ambayo ni Jumapili, siku inayofuata baada ya sabato (Matendo 2:1). Roho Mtakatifu alichagua kuja Jumapili ili kuanzisha siku mpya ya matumaini ya kumwabudu Mungu katika Roho na Kweli (Yohana 4:23-24).
5. Siku ya Pentekoste yaani Jumapili, ndiyo siku ya kwanza ambayo kanisa la kwanza la Mitume lilianza mahubiri kwa nguvu ya Roho Mtakatifu, na watu 3,000 wakaokoka na kubatizwa na kuanza kusanyiko la kwanza la ibada kanisani (Matendo 2:1-41). Torati ilipotambulishwa ilisababisha kuuawa kwa watu wengi sana, lakini neema na kweli ilipotambulishwa ilisababisha kuokolewa kwa watu wengi sana.
6. Wakristo wa Kanisa la kwanza la Mitume walikusanyika katika ibada siku ya kwanza ya juma yaani Jumapili (1Wakorintho 16:1-2). Mtume Paulo alifundisha katika ibada iliyofanyika siku ya kwanza ya Juma yaani Jumapili (Matendo 20:7-12). Neno linatuagiza kumfuata Paulo kama yeye anavyomfuata Kristo (1 Wakorintho 11:1), hivyo na sisi hatuna budi kufanya kusanyiko siku ya Jumapili. Pia ni muhimu kufahamu kuwa kanisa limejengwa chini ya msingi wa Mitume na Manabii na Kristo akiwa jiwe kuu la pembeni. Hivyo walichofanya Mitume na Manabii wa Yesu ndivyo nasi tunapaswa kufuata.
   Lakini hata hivyo Wakristo halisi tunapaswa kujifunza Neno la Mungu na kumwomba Mungu kila siku na siyo Jumapili tu. Mitume walidumu ndani ya hekalu kila siku; (Matendo 2:46) tunasoma, “Na siku zote kwa moyo mmoja walidumu ndani ya hekalu, wakimega mkate nyumba kwa nyumba….”

MAREKEBISHO YA SHERIA KATIKA AGANO JIPYA
KUPITIA CHEKECHO LA MSALABA
  Mungu habadiliki katika tabia na sifa zake, lakini Yeye mwenyewe amekuwa akiweka amri na kuzibadili kama apendavyo Yeye, katika vizazi mbalimbali. Na pia amekuwa akifanya maagano na vizazi mbalimbali kwa kadiri ya kusudi lake.
  Adamu na Hawa hawakupewa torati, bali walipewa amri moja tu, yaani kutokula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya kama Biblia inavyosema katika kitabu cha Mwanzo 2:16-17. Mungu hakumpa Adamu amri ya ‘usizini’ kwa kuwa hakuwapo mwanamke mwingine ila mkewe Hawa. Vivyo hivyo hakumpa amri ya ‘usiibe’ kwa kuwa vitu vyote vilivyo kuwapo katika bustani ya edeni alipewa na Mungu kuwa vyake. Pia Mungu asingeweza kumwambia Adamu aheshimu wazazi wake kwa kuwa hawakuwapo. Katika maandiko hatuoni Mungu akimwagiza Adamu ashike sabato. Kwa hiyo zama za Adamu na Hawa walipewa amri moja tu.
  Tukija zama za Nuhu, tunaona Nuhu naye anafanya agano na Mungu na kupewa sheria zifuatazo katika Mwanzo 9:1-7; sheria ya kwanza Nuhu anaambiwa asile nyama pamoja na uhai wake yaani damu (Mwanzo 9:4-5), na sheria ya pili, Nuhu na kizazi chake wanakatazwa kuua (Mwanzo 9:6).
  Tukija kwa Ibrahimu tunaona Mungu anafanya agano na Ibrahimu na kumwambia awe mkamilifu (Mwanzo 17:1). Lakini pia anampa sheria mpya ya kutahiri nyama ya magovi yao, kitu ambacho Nuhu hakuamriwa kufanya.
  Baada ya kuja uzao wa Yakobo yaani wana wa Israeli, tunaona wanapewa torati na hukumu kupitia Musa. Hivyo basi, Mungu amekuwa akitoa amri na kuzibadili kizazi hadi kizazi. Kubadilika kwa sheria kulingana na nyakati si kitu kigeni, hayo ni mapenzi yake na hakuna mwanadamu wa kuhoji. Kazi yetu wanadamu kama watekelezaji wa amri za Mungu, ni kuwa na akili na kufahamu nyakati tulizo nazo, na amri zipi tunapaswa kuzitenda katika nyakati hizi tulizo nazo. Maadiko katika kitabu cha 1 Nyakati 12:32 yanasema, “Na wana wa Isakari, watu wenye akili za kujua nyakati, kuyajua yawapasayo Israeli wayatende; vichwa vyao walikuwa watu mia mbili na ndugu zao wote walikuwa chini ya amri yao.” Siyo kwa sababu Ibrahimu aliambiwa na Mungu kutahiri mtoto wa kiume wa siku nane, na sisi katika Agano jipya tufanye hivyo, la hasha.
   Leo sisi hatumo katika maongozi ya Agano la kale likiongozwa na torati, bali tumo katika maongozi ya Agano jipya tukiongozwa na sheria ya Kristo (Wagalatia 6:2) na siyo na torati ya Musa.

MAREKEBISHO YA SHERIA KATIKA AGANO JIPYA
   Marekebisho ya sheria katika Agano jipya, inajumuisha vitu vifuatavyo; kwanza, kupitishwa kwa baadhi ya sheria kutoka katika Agano la kale kama zilivyo; pili, kupitishwa kwa sheria za Agano la kale baada ya kufanyiwa maboresho; tatu, kutopitishwa kabisa kwa baadhi ya sheria za Agano la kale, sheria hizo ni kama kushika sabato, makatazo ya baadhi ya vyakula pamoja na kuondolewa kwa hukumu; na nne, kuwekwa kwa sheria mpya.
    Katika kutopitishwa kabisa kwa baadhi ya sheria katika Agano la kale, Bwana Yesu, aliziondoa sheria ambazo zilikuwa ni kivuli yaani zilizoashiria kitu fulani kijacho, mfano sabato (pumziko) ilikuwa ni kivuli au ishara iliyomwashiria kuja kwa Bwana Yesu ambaye ndiye pumziko halisi, ni kwa sababu hiyo basi, kushika sabato katika Agano jipya kuliondolewa na chekecho la msalaba, kwa kuwa sheria hii ilimwakilisha Bwana Yesu mwenyewe kama pumziko halisi (sabato). Hivyo kwa vile pumziko (sabato) mwenyewe amekuja, haina haja ya kuendelea kushika kivuli au ishara.
   Pia kuna sheria za Agano la kale ambazo zimepita katika Agano jipya lakini baada ya Bwana Yesu, kuzifanyia marekebisho kwa kuziboresha, yaani kuziweka kiroho zaidi. Kwa ujumla sheria kuu katika torati, ambazo ziligoma kupita kwenye chekecho la msalaba ni Kushika sabato, sheria ya makatazo ya vyakula na hukumu za torati. Kuhusu sabato, Bwana Yesu hakushika sabato na wala hakuwaruhusu wanafunzi wake kushika sabato kama tulivyokwisha kuona hapo nyuma kwa upana sana(Marko 2:23-28; Yohana 9:16; Yohana 5:16-18); Pia katika torati walikatazwa kula baadhi ya vyakula yaani wanyama n.k, lakini katika Agano jipya, Bwana Yesu aliwaagiza mitume wake wale chochote watakachowekewa mbele yao, tena wale bila kuuliza, maandiko yafuatayo yanatupa mwongozo wa kula vyakula vyote (Luka 10:8; Marko 7:18-20; Mathayo 15:11; Tito 1:15; Wakolosai 2:16; 1 Timotheo 4:3-5; Warumi 14:14, 20; Matendo 11:6-9); Kadhalika kuhusu hukumu walizopewa wana wa Israeli nyakati za Musa, Bwana Yesu alipokuja, aliziondoa kwa kusema, “Msihukumu msije mkahukumiwa.” (Mathayo 7:1-2; Luka 6:37).
   Katika Mathayo 5:21-43 tunaona Bwana Yesu akifanya marekebisho ya sheria kwa uwazi kabisa tena mbele za watu, Mathayo 5:21-22Mmesikia watu wa kale walivyowaambia, Usiue…..Bali mimi nawaambieni…..” Bwana Yesu hapa anairekebisha sheria kwa kuiboresha. Mathayo 5:27-28, “Mmesikia kwamba imenenwa, Usizini, lakini mimi nawaambia kila amtazamaye mwanamke kwa kumtamani, amekwisha kuzini naye moyoni…Mathayo 5:31-32, “Imenenwa pia, mtu akimwacha mkewe, na ampe hati ya talaka; lakini mimi nawaambia kila mtu amwachaya mkewe……..” Kwa ujumla ukisoma Mathayo 5:21-43 yote utaona jinsi Bwana alivyofanya marekebisho ya sheria.

KUHANI MPYA NA SHERIA MPYA
   Moja ya utofauti kati ya Agano la kale na Agano jipya ni ukuhani. Katika Agano la kale Kuhani alikuwa ni mwanadamu ambaye ni Haruni na uzao wake (mdhambi). Lakini katika Agano jipya kuhani ni Mungu mwenyewe yaani Yesu Kristo (Mkamilifu).Na maandiko katika kitabu cha Waebrania 7:12 yanasema, “Maana ukuhani ule ukibadilika, hapana budi sheria nayo ibadilike”  Kuhani wa Agano la kale alikuwa ni kuhani wa sheria ya amri iliyo ya jinsi ya mwili, lakini kuhani wa Agano jipya ambaye ni Yesu Kristo, Yeye ni kuhani wa sheria ya nguvu za uzima usio na ukomo kama Neno la Mungu linavyosema katika Waebrania 7:16, “Asiyekuwa kuhani kwa sheria ya amri iliyo ya jinsi ya mwili, bali kwa nguvu za uzima usio na ukomo.” Kwa hiyo ni dhahiri kabisa, kwamba kwa kuwa kuhani amebadilika na sheria nayo katika Agano jipya imebadilika.

ANGALIZO KWA WANAOSHIKA SHERIA YA SABATO
   Kushika sabato, makatazo ya vyakula au vinywaji na hukumu, ni miongoni mwa amri katika torati ya Musa. Na amri hizi, Bwana Yesu, hakuzipitisha katika Agano la jipya kama tulivyokwisha kuona katika sura zilizopita. Kwa hiyo, amri hizo, si miongoni mwa sheria za Kristo (Wagalatia 6:2). Kimsingi, unapofundisha au kuishika torati ya Musa, unawapofusha watu wasione kazi ya msalaba, hivyo watu hao watajiita wakristo, lakini ni watu wenye tabia za mwilini. Kadhalika unapofundisha na kuyashika maagizo ambayo yapo kinyume na mmiliki wa mbingu, ambaye ni Bwana Yesu Kristo, ni wazi kabisa huko ni kujiweka au kuwaweka watu karibu na shimo la jehanamu ya moto.
  Kwa kawaida mtu anayeisogelea torati ya Musa (kushika sabato, makatazo ya vyakula na vinywaji), hutafuta tamaa za dhambi na hatimaye mtu huyo huzalia mauti; Warumi 7:5 tunasoma, “Kwa maana tulipokuwa katika hali ya mwili, tamaa za dhambi, zilizokuwapo kwa sababu ya torati, zilitenda kazi katika viungo vyetu hata tukaizalia mauti mazao.”
   Lakini pia, mtu anayeshika torati ya Musa katika nyakati hizi za Agano jipya yaani kushika sabato na makatazo ya vyakula au vinywaji n.k, mtu huyo huitwa mwanafunzi wa Musa na wala si mwanafunzi wa Yesu, kwa kuwa torati ilikuja kwa mkono wa Musa na neema na kweli kwa mkono wa Kristo (Yohana 1:17). Hata kama mtu anamtaja Bwana Yesu, na mtu huyo akawa anashika sheria za Musa yaani kushika sabato makatazo ya vyakula au vinywaji n.k, bado mtu huyo ataendelea kutafunwa na nguvu ya torati. Na zifuatazo ni dalili za mtu anayemtaja Yesu lakini bado nguvu ya torati inamtafuna;
1.      Mtu huyu huwa na tabia ya unafiki (nje huonekana ni mtakatifu lakini rohoni ni mdhambi)-Mathayo 6:2; Mathayo 23:25-28. Mafarisayo walikuwa na tabia hii, hivyo na mtu anayeshika torati atakuwa na tabia hii.
2.      Mtu huyu huwa na tabia ya kupenda kubishana, kwa kuwa torati inamfanya asiwe rohoni. Hushawishika kwa hekima yenye kushawishi akili na si kwa dalili za roho na nguvu (1 Wakorintho 2:4-5).
3.      Mtu huyu huwa na tabia ya kujihesabia haki, wakati wote hujiona sahihi, wakati amepotea, nguvu ya torati humpofusha asione ukweli (Mathayo 7:1-2).
4.      Mtu wa namna hii, huwa na tabia ya kuinadi sheria moja ambayo anaimudu kuishika, mfano, anaweza kuwa mtu huyo anashika sana sheria ya sabato, basi atainadi hiyo sabato kuliko kumnadi Kristo. Hata kama atamwona mtu anafanya uasherati, ili mradi anashika sabato, huyo kwake ni mtakatifu.
5.      Mtu wa namna hii huwa na tabia ya kuwaudhi walio zaliwa kwa roho yaani waliookoka; Wagalatia 4:29 tunasoma, “Lakini kama vile siku zile yule aliyezaliwa kwa mwili alivyomwudhi yule aliyezaliwa kwa Roho, NDIVYO ILIVYO NA SASA.”
6.      Mtu huyu huwa na juhudi ya kumtumikia Mungu lakini si katika Roho na kweli, hivyo huwafanya waongofu wawe wana wa jehanamu mara mbili (Mathayo 23:15).
7.      Mtu wa namna hii huwa na wema wa kujionesha mbele za watu na si wema halisi (Mathayo 6:1).
8.      Ni ngumu mtu wa namna hii kushinda dhambi, kwa sababu ya nguvu ya torati inayomkalia kutenda dhambi.

   Ukifanya uchunguzi wa kina, utagundua kuwa, waanzilishi wa dhehebu la wanaoshika sabato, hawakuwa wanatheolojia na watu waliojua maandiko; na wala hawakukaa chini ya mafundisho ya wachungaji wao. Mwanzilishi wa Kwanza ni Mmarekani aitwaye William Miller, alizaliwa Pittsfield, Massachusetts, mwaka 1782 na kufariki mwaka 1849. Mtu huyu aliacha ukristo, lakini baadaye aliamua kurudi tena kwenye ukristo mwaka 1816, na ndiye aliyeleta mafunuo ya uongo ya kurudi kwa Bwana Yesu mwaka 1844, hata kusababisha hasara na mtafaruku mkubwa sana miongoni mwa wafuasi wake (Wana majilio-Adventists). Mwanzilishi wa pili ni Hiram Edson, huyu alikuwa ni mfuasi wa Miller, na ndiye aliyechangia mafundisho potofu ya hukumu ya upelelezi kwenye dhehebu hilo, baada ya unabii wao wa kurudi kwa Yesu kutotimia. Mwanzilishi wa tatu ni aliyekuwa baharia zamani, mtu aitwaye John Bates, huyu bwana ndiye aliyetoa mchango mkubwa wa kurudisha sabato ya Agano la kale.  Na ndiye wa kwanza kutoa mafundisho ya uongo kwamba, Jumapili ni alama ya mnyama, bali siku ya sabato ndiyo muhuri wa Mungu kwa watu wake walio waaminifu. Mwanzilishi wanne ni Bwana James na mke wake aitwaye Ellen Gould White, hawa ndiyo waliouendeleza usabato kuliko mtu mwingine yeyote. James na mkewe walijiunga na Miller mwaka 1840 na 1842 na hii iliwapelekea kutengwa na kanisa lao la Methodist. Ellen ndiye aliyekuja kuyakazia mafundisho ya kushika sabato, baada ya kudai kuwa alipelekwa mbinguni na kukuta katika amri kumi za Mungu amri ya nne ya kushika sabato, ilikuwa iking’aa kuliko zote.
   Kimsingi, hawa wote hawakuwa watu walioijua Biblia bali walienda kwa nguvu ya upeo mdogo wa kimaandiko waliokuwa nao. Kubwa zaidi ni nguvu ya pesa katika kueneza mafundisho, na hata kufanya kusambaa sehemu kubwa hususani Afrika.
   Watoto wa Mungu, ni lazima tutambue kuwa sisi sote tumeokolewa kwa neema, na wala si kwa matendo ya sheria (Waefeso 2:8-9). Kama tutaishi kwa kufuata mambo ya mwili, hapo tunataka kufa, bali kama tutayafisha matendo ya mwili kwa roho, hapo tutaishi, kwa kuwa wanaongozwa na Roho, hao ndiyo wana wa Mungu (Warumi 8:13-14).

Godwin Gunewe